1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani yataka ujasusi wa Marekani ukome

Mohammed Khelef/dpa/AFP11 Julai 2014

Ujerumani imeitolea wito Marekani kuchukua jitihada binafsi za kurekebisha upya hali ya mahusiano kati ya pande hizo mbili baada ya kile serikali ya Ujerumani inachokiita "kuvunjwa kwa uaminifu".

https://p.dw.com/p/1Cakl
Waziri wa Sheria wa Ujerumani, Heiko Maas (kulia) na mwenzake wa Mambo ya Ndani, Thomas de Maizière.
Waziri wa Sheria wa Ujerumani, Heiko Maas (kulia) na mwenzake wa Mambo ya Ndani, Thomas de Maizière.Picha: picture-alliance/dpa

Akizungumza na gazeti la Passauer Neuen Presse hivi leo, Waziri wa Sheria wa Ujerumani, Heiko Maas, amesema serikali yake inataka uhakikisho kutoka Marekani kwamba nchi hiyo haitafanya tena ujasusi dhidi ya Ujerumani.

Gazeti la Bild limevinukuu vyanzo kadhaa vya habari serikalini vikisema tayari serikali imeyaamuru mashirika yake ya usalama kupunguza ushirikiano wao na Marekani kufikia kiwango cha chini kabisa hadi yatakapopokea agizo jengine.

Magazeti na vyombo kadhaa vya habari hivi leo vimeamka na kauli zinazounga hatua hizi kali za serikali dhidi ya kile vinachokiita kuwa "ujeuri mkubwa wa Marekani" kwa Ujerumani.

Gazeti la Sueddeutsche Zeitung limekiita kitendo cha hapo jana cha serikali ya Ujerumani kumfukuza mkuu wa ofisi ya Shirika la Ujasusi la Marekani, CIA, kuwa ni "mwanzo mpya", huku gazeti la kihafidhina la Frankfurter Allgemeine Zeitung likiandika: "Merkel si kizulia cha Obama. Ujumbe ambao Merkel amemtumia ni muhimu na hauna utata. Ni juu ya Wamarekani kuuelewa ama la."

Von der Leyen aja juu

Yumkini ni kauli ya Waziri wa Ulinzi, Ursula von der Leyen, ndiyo kali zaidi kuwahi kutolewa na viongozi wa ngazi za juu wa serikali ya Kansela Angela Merkel kuhusiana na tuhuma hizi za Marekani kufanya ujasusi dhidi ya taifa ambalo tangu enzi za Vita vya Pili vya Dunia limekuwa rafiki wa karibu.

Waziri wa Ulinzi wa Marekani, Ursula von der Leyen.
Waziri wa Ulinzi wa Marekani, Ursula von der Leyen.Picha: picture-alliance/dpa

"Ushirikiano wetu mzuri na ubadilishanaji wa taarifa kati ya mashirika yetu ya usalama umefanikisha kuzuia njama nyingi za mashambulizi na kutusaidia kuokoa maisha. Lakini tunahitaji mahusiano yenye heshima na hivyo ni bora kuona imani hii inarejeshwa. Serikali imetoa funzo zuri na kuonesha kwamba haitavumilia kamwe uvunjwaji wa uaminifu na tunapaswa kurekebisha mambo." Amesema von der Leyen.

Marekani yakwepa

Hata hivyo, akizungumzia kadhia hiyo ya kufukuzwa kwa afisa wao wa ujasusi na serikali ya Ujerumani, msemaji wa wizara ya mambo ya kigeni ya Marekani, Jen Psaki, ameepuka kuingia undani ingawa akasisitiza ushirikiano wa kati ya pande hizo mbili ni muhimu sana, na kwamba suala hilo litazungumziwa kwenye ngazi ya mawaziri.

"Ninatazamia kuwa Waziri Kerry na mwenzake wa Ujerumani, Steinmeier, watakuwa na fursa ya kuzungumzia hili hivi karibuni. Lakini nitarejelea tu kuwa mahusiano yetu na Ujerumani ni muhimu sana kabisa. Tuna maeneo mengi ya kushirikiana. Bila ya shaka tuna maeneo ambayo pia hatukubaliani, lakini ishara ni kwamba mahusiano imara yanaweza kushinda suintafahamu au changamoto hizo, na tutaendelea kufanya hivyo kupitia njia muafaka," msemaji huyo aliwaambia waandishi wa habari jana.

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani, Jen Psaki.
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani, Jen Psaki.Picha: SAUL LOEB/AFP/Getty Images

Kashfa hii imeyatikisa mahusiano kati ya Berlin na Washington katika kiwango ambacho hakijawahi kushuhudiwa tangu mtangulizi wa Kansela Merkel, Gerhard Schroeder, kupinga uvamizi wa Marekani dhidi ya Iraq mwaka 2003.

Imebainika kuwa hata Kansela Merkel mwenyewe, aliyezaliwa na kukulia kwenye iliyokuwa Ujerumani Mashariki, alikuwa mmoja ya maelfu ya Wajerumani ambao simu zao za mkononi zimekuwa zikitegwa na majasusi wa Kimarekani.

Mhariri: Saumu Yusuf