1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroIran

Biden aitahadharisha Iran kutoishambulia Israel

13 Aprili 2024

Rais Joe Biden wa Marekani ameirai Iran kutoishambulia Israel akisema utawala mjini Washington umejitolea kuilinda nchi hiyo na kwamba hujuma zozote kutoka Tehran hazitafanikiwa.

https://p.dw.com/p/4eigO
Rais Joe Biden wa Marekani
Rais Joe Biden wa MarekaniPicha: DW

Biden ametoa matamshi hayo wakati akizungumzia uwezekano wa Iran kufanya mashambulizi ya kulipa kisasi kufuatia hujuma dhidi ya jengo lake la ubalozi nchini Syria lilitokea Aprili Mosi.

Iran pamoja na Marekani zinaamini kuwa Israel ndiyo ililishambulia jengo hilo, mkasa uliosababisha vifo vya makamanda wawili na maafisa wengine kadhaa wa jeshi la Iran.

Tangu wakati huo watawala mjini Tehran, akiwamo Kiongozi Mkuu Ayatollah Ali Khamenei, wameapa kulipiza kisasi wakisema Israel imefanya "kosa kubwa na ni lazima iadhibiwe".

Tathmini iliyotolewa na Biden inaonesha Iran inapanga kuishambulia Israel hivi karibuni lakini ameitahadharisha kutochukua hatua hiyo.