1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Watu 9 wauawa Ukraine katika shambulizi la Urusi

19 Aprili 2024

Watu tisa wameuawa katika shambulizi la Urusi nchini Ukraine mapema hii leo huku Kyiv ikisema kuwa imefanikiwa kuindungua ndege ya kijeshi ya Urusi kusini mwa nchi hiyo, madai yaliyonakushwa na Moscow.

https://p.dw.com/p/4exsv
Ukraine
Eneo la Dnipropetrovsk nchini Ukraine limeendelea kushambuliwa kwa makombora na jeshi la Urusi Picha: Dnipropetrovsk Regional Military Civil Administration via Telegram/Handout via REUTERS

Watu tisa wameuawa katika shambulizi la Urusi nchini Ukraine mapema hii leo huku Kyiv ikisema kuwa imefanikiwa kuindungua ndege ya kijeshi ya Urusi kusini mwa nchi hiyo, Ingawa Wizara ya Ulinzi huko Moscow imekanusha na kusema kwamba huenda ndege hiyo ya kijeshi ilipata hitilafu za kiufundi. 

Urusi imekiri kuanguka kwa ndege yake ya kijeshi mapema leo katika eneo la kusini mwa Ukraine wakati ikirejea kambini baada ya kufanya mashambulizi yaliyowaua watu 9 na wengine 20 kujeruhiwa.

Soma zaidi. Wanachama wa NATO watakiwa kuitikia wito wa Ukraine

Ukraine kwa upande wake imesema kwa mara ya kwanza tangu kuanza kwa vita vya Urusi nchini Ukraine mwaka wa 2022 kuwa imefaulu kuidungua ndege ya kijeshi ya Urusi iliyokuwa inarusha makombora.

Ukraine imesema kudunguliwa kwa ndege hiyo ya kudondosha makombora ni ishara tosha ya ushindi kwa Ukraine ambayo imekumbwa na msururu wa mashambulizi ya anga kutoka kwa Urusi kwa zaidi ya miaka miwili.

Ukraine | Dnipro
Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky amerejea mwito wake kwa washirika wake wa magharibi kuisaidia nchi hiyo msaada wa haraka wa mifumo ya ulinzi wa angaPicha: Ukrainian Presidentia/ZUMA//IMAGO

Katika taarifa iliyochapishwa katika mtandao wa kijamii wa Telegram, Ofisi ya mwendesha mashtaka mkuu ya Ukraine imesema shambulizi hilo lilitokea katika eneo la mashariki la Dnipropetrovsk limeharibu majengo na idadi ya waathirika inaweza kuongezeka.

Zelensky: Tunahitaji msaada wa mifumo ya ulinzi

Baada ya shambulizi hilo, Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky amerejea mwito wake kwa washirika wake wa magharibi kuisaidia nchi hiyo msaada wa haraka wa mifumo ya ulinzi wa anga.

Ingawa hapo jana, Katibu Mkuu wa Jumuiya ya nchi ya kujihami NATO Jens Stoltenberg alisema kwenye mkutano wa nchi tajiri duniani za G7 huko Italia kwamba jumuiya hiyo inafanya kila jitihada kuweza kuisaidia nchi hiyo mifumo ya ulinzi.

NATO
Katibu Mkuu wa NATO Jens StoltenbergPicha: Kenzo Tribouillard/AFP

  "Tutazingatia leo suala la ulinzi wa anga. Kuna hitaji muhimu la dharura la ulinzi wa anga. Sasa unashughulikia hilo kwenye jumiya ya NATO, tangu Waziri wa Mambo ya Nje wa Ukraine Dmytro Kuleba  alipohudhuria mkutano wetu wa Mawaziri wa Mambo ya Nje, wiki mbili tu zilizopita huko Brussels. Kwa hivyo tumeongeza takwimu kuhusu mifumo tofauti ya ulinzi wa anga tuliyonayo katika NATO, na kuzingatia mifumo ya Patriot, na tunafanya kazi na washirika kuhakikisha kwamba wanapeleka tena mifumo mingine zaidi nchini Ukraine.''amesema Jens Stoltenberg.

Soma zaidi. Waziri wa uchumi wa Ujerumani Robert Habeck awasili Ukraine

Jeshi la anga la Ukraine limetoa taarifa kwamba Urusi ilirusha makombora 22 na droni 14 zilizotengenezewa Iran, huku taarifa hiyo ikisema makombora 15 yaliweza kudunguliwa.

Mashambulizi ya Urusi nchini Ukraine yameathiri maeneo mengi ya Ukraine tangu yalipozuka miaka miwili iliyopita, Mapema wiki hii watu 18 waliuawa katika shambulio katika mji wa kaskazini wa Chernegiv.


Mwandishi: Suleman Mwiru