1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wakuu nchi za EAC wajadili mabadiliko ya tabia nchi

Veronica Natalis
24 Novemba 2023

Wakuu wa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki wanakutana Arusha, Tanzania, kujadili mustakabali wa jumuiya na wameyata mataifa ya Afrika kukabiliana na chanagmoto zilizopo ikiwemo athari za mabadiliko ya tabia nchi.

https://p.dw.com/p/4ZOKl
Tanzania | Viongozi wa nchi za Jumuiya ya Afrika mashariki
Viongozi wa nchi za Jumuiya ya Afrika mashariki katika mkutano wa mabadiliko ya tabia nchi na usalama wa chakula.Picha: Philbert Rweyemamu/EAC

Mkutano huo wa kilele ulioanza jana umewaleta pamoja viongozi wakuu wa nchi 7 wanachama wa jumuiya hiyo huku ajenda za majadilino zikiwa ni  mabadiliko ya tabia nchi na usalama wa chakula.

Wakijadili athari za mabadiliko ya tabia nchi zinazoyakumba mataifa hasa ya Afrika wakuu hao wa nchi wametilia mkazo kwamba Afrika haitakiwi kutegemea  misaada ya pesa za mazingira kutoka kwa mataifa yaliyoendelea ambayo ndio yanayolaumiwa pakubwa kwa uchafuzi wa mazingira kwa kutoa hewa chafu.

Katika hotuba yake  Rais wa Tanzania Samia Suluhu ameyatupia lawama mataifa hayo kwa kuchelewesha ama kushindwa kabisa kutekeleza ahadi ya kuzisaidia kiuchumi nchi za Afrika ili kuhimili athari za mabadiliko ya tabia nchi. 

"Nadhani ni wakati muafaka kwa sisi waafrika, kuacha kutegemea watu wengine kwenye ufadhili wa sala la mabadiliko ya tabia nchi." Alisema rais Samia.

Soma pia:Djibouti na Ethiopia zinatarajia kujiunga na Jumuiya ya EAC

Katika upande wa usalama wa chakula mkutano huo umegusia mambo kadhaa ikiwa ni pamoja nakuimarisha mifumo ya chakula kwa kutumia maliasili zilizopo miongoni mwa nchi wanachama.

Kuimarisha na kuweka mkazo katika kilimo cha kisasa cha umwagiliaji na kinachostahimili hali ya hewa.

Nishati endelevu miongoni mwa hoja muhimu

Suala la nishati lilikuwa pia ni miongoni mwa ajenda zilizotawala mkutano huo wa 23 wa wakuu wa nchi wa jumuia ya Afrika mashariki wakikubaliana kwa kauli moja mamtumizi ya nishati mbadala ili kuendeleza mwitikio wa utunza mazingira. 

Rebecca Kaganda Naibu Waziri mkuu wa Uganda akimwakilisha Rais Yoweri Museven amesema, ni wakati wa wananchama kuunganisha nguvu katika kutumia rasilimali zilizopo. 

Mkutano wa nchi za Jumuiya ya Afrika mashariki kuhusu mabadiliko ya tabia nchi na usalama wa chakula.
Mkutano wa nchi za Jumuiya ya Afrika mashariki kuhusu mabadiliko ya tabia nchi na usalama wa chakula.Picha: Philbert Rweyemamu/EAC

"Tunakakiwa kushirikiana na mashirika binafsi na wadau wengine ili kuwa na aina ya kilimo kinachoweza kutupa uhakika wa chakula kwa muda mrefu."

Akitolea mgano taifa lake Uganda, amesema wanao mpango wa wa miaka 10 wa utunzaji wa mazingira, wakibainisha maeneo mbali mbali kwaajili ya mikakati ya utunzaji wa mazingira pamoja na kutoa  elimu kwa watu wanaoishi porini maeneo ya vijijini. 

Soma pia:Somalia yajadiliwa kujiunga na jumuiya ya Afrika Mashariki

Mkutano huo uliotanguliwa na mkutano wa  44 wa baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki  bado unaendelea jijini Arusha na marais waliohudhuria ni pamoja na Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassa, Rais wa Kenya William Ruto pamoja na Rais wa Burundi Evariste Ndayishimiye ambaye pia ni mwenyekiti wa zamu wa wakuu wa nchi za jumuiya ya Afrika Mashariki.

Nchi zilizotuma wawakilishi ni Sudan Kusini, Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo,  Rwanda iliyowakilishwa na waziri mkuu wake Edouard Ngirente, pamoja na jamhuri ya Uganda iliyowakilishwa na naibu waziri mkuu wake Rebecca Kaganda.

Miongoni mwa matukio yanayotarajiwa katika siku ya pili ya mkutano huo hii leo ni pamoja na Somalia kuidhinishwa kuwa mwanachama mpya wa Afrika Mashariki, mjadala juu ya maendeleo ya ripoti ya Jumuiya  hiyo kuhusu kurejesha amani mashariki mwa Jamhuri ya kidemokrasia ya Kongo pamoja na Rais wa Sudan Kusini Salva Kiir kupewa uenyekiti wa Jumuiya hiyo.  

Kikosi cha EAC chatakiwa kuondoka Congo