1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Upinzani waanza maandamano ya kumtaka Pashinyan kujiuzulu

Bruce Amani
4 Mei 2022

Vyama vya upinzani nchini Armenia leo vimeanza tena maandamano ya mitaani katika mji mkuu Yerevan katika jaribio la kumuondoa madarakani Waziri Mkuu Nikol Pashinyan.

https://p.dw.com/p/4Aod4
Armenien Oppositionskundgebung
Picha: IMAGO/SNA

Vyama vya upinzani nchini Armenia leo vimeanza tena maandamano ya mitaani katika mji mkuu Yerevan katika jaribio la kumuondoa madarakani Waziri Mkuu Nikol Pashinyan kutokana na jinsi anavyoushughulikia mzozo wa mpaka na Azerbaijan.

Maelfu ya wafuasi wa upinzani wameandamana tangu Jumapili, huku wakizifunga kwa muda barabara za katikati ya mji mkuu Yerevan katika kampeni ya kumshinikiza Pashinyan kujiuzulu.

Viongozi wa upinzani wanamtuhumu kwa kupanga njama ya kuiachia Azerbaijan eneo zima linalogombaniwa la Nagorno-Karabakh ambalo nchi hizo mbili hasimu zilipigana vita viwili, katika mwaka wa 2020 na katika miaka ya 1990.

Kiongozi wa upinzani na makamu spika wa bunge Ishkhan Saghatelyan amesema maandamano yataongezeka na kuendelea hadi Pashinyan atakapojiuzulu. Amesema upinzani unapanga kutangaza serikali ya mpito inayowajumuisha wasomi wasioegemea vyama vya kisiasa.