1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais wa Iran alisifu jeshi kulipiza kisasi kwa Israel

Saumu Mwasimba
19 Aprili 2024

Rais Ebrahim Raisi wa Iran amesifu hatua iliyochukuliwa na jeshi la nchi yake kulipiza kisasi dhidi ya mashambulio yaliyofanywa na Israel katika ubalozi wake mdogo, mjini Damascus, Syria.

https://p.dw.com/p/4ezMd
Russland | Sitzung der russischen Staatsduma | Iranischer Präsident Ebrahim Raisi
Rais Ebrahim Raisi wa Iran (katikati) kwenye picha hii iliyopigwa mwezi Januari 2021 nchini Urusi.Picha: Anton Novoderezhkin/TASS/dpa/picture alliance

Akiwahutubia mamia ya wananchi wa Iran katika mkoa wa Semnan siku ya Ijumaa (Aprili 19), kiongozi huyo hakugusia chochote kuhusu miripuko iliyotokea usiku  karibu na mji wa Isfahan. 

Kwa mujibu wa ripoti za shirika la habari la Tasnim, Mkuu wa Majeshi wa Iran Abdolrahim Mousavi amezungumzia tukio hilo la Isfahan kwa kusema mifumo ya ulinzi wa anga ilikidunguwa kifaa kinachotiliwa mashaka, na hakuna uharibifu uliotokea.

Soma zaidi: Hofu yaongezeka Mashariki ya Kati baada ya Israel kuishambulia Iran

Hata hivyo, mkuu huyo wa jeshi la Iran alisema uchunguzi ulikuwa unaendelea kutathmini ukubwa wa tukio hilo.

Kwa upande mwingine, msemaji wa idara inayohusika na masuala ya anga za mbali, Hossein Dalirian, alisema aina fulani ya droni iliyojaribu kuruka kwenye anga la Iran ilidunguliwa, lakini hakuna shambulio lolote la anga kutoka nje ya mipaka yake lililofanyika Isfahan au kwengineko katika nchi hiyo.