1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Navalny afariki dunia gerezani Urusi

Tatu Karema
16 Februari 2024

Kiongozi wa upinzani wa Urusi na mkosoaji mkubwa wa Rais Vladmir Putin, Alexei Navalny mwenye umri wa miaka 47 amefariki dunia leo asubuhi akiwa katika gereza moja nchini humo.

https://p.dw.com/p/4cUKb
Alexei Navalny
Kiongozi wa upinzani wa Urusi, Alexei Navalny, amefariki dunia akiwa gerezani siku ya Ijumaa (Februari 24).Picha: Pavel Golovkin/AP Photo/picture alliance

Idara ya Magereza ya Urusi ilisema Navalny alijihisi mgonjwa baada ya matembezi asubuhi ya Ijumaa (Februari 16) na kupoteza fahamu.

Idara hiyo iliongeza kuwa juhudi za kumpatia matibabu ya dharura hazikufanikiwa na akafariki dunia.

Navalny alikuwa akitumikia kifungo cha zaidi ya miaka 30.

Soma zaidi: Urusi yamkamata mkosoaji mwingine wa Kremlin

Msemaji wa Ikulu ya Kremlin, Dmitry Peskov, alisema Rais Vladimir Putin tayari alikuwa amejulishwa kuhusu kifo hicho na kwamba ni jukumu la madaktari kufafanua sababu yake. 

Ofisi yake haijajulishwa

Alexei Nawalny, 2010
Picha ya Alexei Navalny ya mwaka 2010 kabkla ya kukamatwa na kufungwa jela na utawala wa Rais Putin.Picha: Alexander Zemlianichenko/AP Photo/picture alliance

Hata hivyo, katibu wa habari wa Navalny, Kira Yarmysh, alisema yeye na timu yake hawajafahamishwa kuhusu kifo hicho cha Navalny.

Kamati ya Uchunguzi ya Urusi imesema imeanzisha uchunguzi kuhusu kifo hicho.

Soma zaidi: Kiongozi wa upinzani Urusi Alexei Navalny ahukumiwa miaka mingine 19 jela

Viongozi wa ulimwengu wanaendelea kutuma salamu za rambirambi kufuatia kifo cha Navalny wakisema Rais Putin anapaswa kuwajibishwa kufuatia kifo hicho.

Nchi za Magharibi zinasema mwanasiasa huyo aliyatoa muhanga maisha yake ili kupigania demokrasia na uongozi bora.