1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Magharibi waisihinikiza China kuhusu haki za binadamu

Amina Mjahid
23 Januari 2024

Mataifa ya Magharibi, yameishinikiza China kuangalia upya rekodi yake ya haki za binaadamu, ili kuchukua juhudi zaidi kuridhia uhuru wa kujieleza.

https://p.dw.com/p/4bbDc
Uswisi | China UN Geneva
Wakuu wa ujumbe wa China katika Umoja wa Mataifa wakiwa mjini Geneva kutetea rekodi ya haki za binadamu ya taifa hilo.Picha: Fabrice Coffrini/AFP/Getty Images

Mataifa ya Magharibi, yametumia kikao cha kawaida cha Umoja wa Mataifa cha mapito ya rekodi ya haki za binadamu ya China, kuishinikiza Beijing kufanya juhudi zaidi kuruhusu uhuru zaidi wa kujieleza, kulinda haki za jamii za wachache na  kufuta sheria ya usalama ya Hong Kong inayowatatiza wanaharakati huru nchini humo.

Balozi wa China mjini Geneva Chen Xu aliongoza ujumbe kutoka wizara 20 za taifa hilo kwa ajili ya kikao hicho cha mapitio chini ya Baraza la Haki za Binaadamu la Umoja wa Mataifa. Amesisitiza hatua zilizopigwa na China kuondoa umasikini, akisema wananchi wake wanashiriki katika uchaguzi wa demokrasia na kusema pia uhuru wa imani za kidini unalindwa.

Soma pia: UN: China na washirika wake wanatumia wingi wao kulindana

"China inaheshimu na kulinda haki za binaadamu kama jambo muhimu katika uendeshwaji wa serikali. China inachukua muelekeo wa kuimarisha haki za binaadamu zinazoendana na wakati na hali ya kitaifa na imepiga hatua za kihistoria katika kufikia hilo. Tunajizatiti kuwapa watu wetu maisha bora zaidi."

Soma pia: Kwa namna gani China itaimarisha sera zake huko Xinjiang?

Leslie Norton balozi wa Canada katika Umoja wa Mataifa ameitaka China kusitisha aina zote za watu kupotezwa na kuwalenga watetezi wa haki za binaadamu pamoja na kuondolewa kwa sheria ya kitaifa ya usalama iliyowekwa na China mjini Hong Kong.