1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mahakama kuu Rwanda yamzuia Ingabire kugombea urais

Saumu Mwasimba
13 Machi 2024

Mahakama moja mjini Kigali nchini Rwanda imesema kiongozi wa upinzani na mkosoaji mkubwa wa serikali,Victoire Ingabire hana uhalali wa kugombea katika uchaguzi ujao wa rais nchini humo utakaofanyika mwezi Julai.

https://p.dw.com/p/4dTfN
Rwanda |Victoire Ingabire
Kiongozi wa upinzani na mkosoaji mkubwa wa serikali ya Rwanda Victoire Ingabire Picha: CYRIL NDEGEYA/AFP

Mahakama moja mjini Kigali nchini Rwanda imesema kiongozi wa upinzani na mkosoaji mkubwa wa serikali,Victoire Ingabire hana uhalali wa kugombea katika uchaguzi ujao wa rais nchini humo utakaofanyika mwezi Julai.

Mahakama hiyo imesema uamuzi huo umepitishwa kutokana na mwanasiasa huyo huko nyuma kukutwa na hatia ya kuhusika na vitendo vya ugaidi na kuyakanusha mauaji ya halaiki.

Mpinzani huyo wa serikali ya rais Paul Kagame,ameliambia shirika la habari la AFP baada ya kutangazwa uamuzi huo na mahakama kuu mjini Kigali,kwamba hakubaliani na kilichoamuliwa akisema ni uamuzi uliopitishwa kisiasa kwasababu  mahakama za nchi hiyo haziko huru.

Ingabire aliwahi kukaa jela miaka minane baada ya kuhukumiwa kifungo cha miaka 15, kabla ya kupewa msamaha wa rais mnamo mwaka 2018.Ingabire: Matumaini ya uhuru wa vyama vya kisiasa Rwanda  

Aliiomba mahakama kuu mjini Kigali imruhusu kugombea urais katika uchaguzi wa Julai 15 licha ya kuwepo sheria inayozuia watu waliowahi kushtakiwa,na kufungwa jela miezi sita au zaidi, kutogombea uchaguzi.