1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jeshi la Uganda latangaza donge nono kuwanasa ADF

4 Desemba 2023

Kufuatia miripuko miwili ya mabomu mjini Kampala mwishoni mwa wiki, vyombo vya usalama nchini Uganda vimetoa onyo kwa umma kuchukuwa hadhari dhidi ya mashambulizi ya kigaidi ya waasi wa kundi la ADF.

https://p.dw.com/p/4ZkrB
Sehemu yalikofanyika mashambulizi mjini Kampala mwaka 2021.
Sehemu yalikofanyika mashambulizi mjini Kampala mwaka 2021.Picha: Hajarah Nalwadda/Xinhua/dpa/picture alliance

Aidha, jeshi limetangaza zawadi ya shilingi milioni ishirini za Uganda kwa atakayetoa taarifa kuhusu washukiwa wawili wanaodaiwa kutumwa na waasi wa ADF kufanya mashambulizi hayo ya kigaidi.

Naibu msemaji wa jeshi la Uganda, Luteni Kanali Deo Akiiki, aliifahamisha DW kuwa mabomu hayo yaliyoripuka katika vitongoji vya Kabalagala na Nabweru yalipangwa kuripuka kwa muda maalum na "ndiyo maana miripuko hiyo ilitokea takriban wakati moja kwenye vitongoji hivyo vinavyotenganishwa kwa takribani kilomita 13."

Soma zaidi: Mauaji ya watalii yazusha wasiwasi Uganda

Hakuna vifo vilitokea katika majaribio hayo ya kigaidi, ila mchuuzi mmoja mwanamke alijeruhiwa kidogo katika mtaa wa Kabalagala huku kuta zikiporomoka kutokana na bomu lililokuwa katika nyumba ya kukodi.

Mwezi Oktoba, serikali za Uingereza na Marekani ziliwatahadharisha raia wake kuhusu uwezekano wa mashambulio ya kigaidi nchini Uganda.