1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Chama cha CCM chatimiza miaka 47 tangu kuasisiwa

5 Februari 2024

Wakati chama tawala nchini Tanzania CCM leo kinaadhimisha miaka 47 tangu kuasisiwa kwake, baadhi ya wachambuzi wana mitazamo tofauti. Wengine wanaona kimeshindwa kufikia muafaka kuhusu upatikanaji wa katiba mpya.

https://p.dw.com/p/4c2nY
Samia Suluhu Hassan | CCM
Mwenyekiti wa CCM na rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan akiongoza kikao cha kamati kuu ya taifa ya chama hicho mjini Dodoma.Picha: CCM office

CCM iliyozaliwa kutokana na muungano wa vyama vya TANU na ASP imeendelea kuzitawala siasa za Tanzania tangu enzi za mfumo wa chama kimoja kilipokuwa  na kauli mbiu "chama kushika hatamu" ambapo taifa hili limo katika mfumo wa vyama vingi.

Mfahamu mwenyekiti wa CCM:Samia Suluhu

Ingawa CCMinajinasibu kuwa chama kilichoota mizizi kuanzia ngazi ya mashinani hadi kwingineko hata hivyo kinatazamwa kama chamsa kinachoendelea kuneemeka kutokana na mifumo ya kiutendaji kuanzia ile yenye sura ya kidola mpaka  mfumo unaopatikana ndani ya katiba.

Soma ripoti hii:CCM Zanzibar wajiandaa kwa uchaguzi mpya

Baadhi ya wafuatiliaji wa mambo wanaona kwamba nguvu kubwa ya chama hicho imetokana na mengi, lakini kubwa zaidi ni mfumo unaotoakana na yale yaliyoko ndani ya katiba, katiba ambayo baadhi ya watendaji wa serikali kama vile wakuu wa mikoa na wilaya wanafungamanishwa moja kwa moja na chama hicho tawala.

Samia Suluhu Hassan na Emmanuel John Nchimbi
Mwenyekiti wa CCM na rais wa Tanzania Samia Suluhu Haasan na katibu mkuu mpya wa CCM Emmanuel John NchimbiPicha: CCM

 Kwa mtazamo wake, mchambuzi  Sammy Ruhuza anesema chama hicho tawala huenda kikawa katika  wakati mgumu katika siku za usoni iwapo uwanja wa kufanya siasa utakuwa sawa na ngvu za dola zikawekwa kando.

“Uchaguzi unapokuwa huru na haki, pale anaposhinda yoyote hata awe CCM awe mpinzani yeyote yule atakayeshinda amshike mkono mwenzake na aridhike kwamba katika hili umenishida.”

Maoni mbele ya meza ya Duara:Miaka 45 ya CCM nchini Tanzania

Ama, chama hicho tawala kinajitazama kama chama kinavyoweza kuzinganga vyema karata, kikiwapanga viongozi wake kuanzia ngazi ya matawi mpaka taifa. Makongamano yake pamoja na hamasa za nyimbo ni eneo lingine linaloongeza ushawishi kwa wananchi

Mabadiliko ya kimfumo na utendaji ndani ya chama, jinsi kinavyoweza kuibua ajenda na kuzitafutia majawabu ni sehemu ya mikakati inayotajwa kukifanya chama hicho kiendelea kuzitawala siasa za Tanzania na kuzidi kushika dola.

Eric Bernard mchambuzi anayefuatilia kwa karibu siasa za chama hicho anasema CCMni chama kinachobadilika kulingana na mahitaji ya wakati hivyo, kuendelea kusalia madarakani kwa muda mrefu ni jambo lisilotiliwa shaka.

“Chama ndani ya miaka 47 kina wenyeviti tofauti tofauti wa chama, kina makatibu wakuu zaidi ya 11 kwa hiyo kila mara kikuona kuna uhitaji wa namna ya kwenda kinabadilisha uongozi wake kuingiza radha na chachu mpya.”

CCM inatimiza miaka 47 ikiwa bado madarakani na katika uchaguzi uliopita wa mwaka 2020, ilifanikiwa kuvuna karibu vitu vyote vya ubunge na kufanya vizuri katika nafasi ya urais.

Samia Suluhu Hassan mwenyekiti wa CCM
Mwenyekiti wa CCM na rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan akiongoza kikao cha kamati kuu ya taifa ya chama hicho mjini DodomaPicha: CCM office

Soma: Rais Samia Suluhu akutana na vyama vya siasa

Hata hivyo, uchaguzi huo ulikosolewa vikali na upinzani waliodai kutawaliwa na vitimbi pamoja na wizi wa kura madai ambayo hata hivyo yalipingwa na chama hicho tawala.

Lakini baadaye mwaka huu, taifa hili litarejea tena katika uchaguzi wa serikali za mitaa na baadaye kufuatiwa na uchaguzi mkuu hapo mwakani na swali linaloanza kugonga vichwa vya wengi ni kwa kiasi gani uchaguzi huo utakuwa huru na haki. Majibu ya swali hilo ndiyo yatabainisha ushawishi wa kweli kwa vyama vyote vya siasa mbele ya wananchi.