1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Baerbock ahofia mpango wa Israel kuushambulia mji wa Rafah

13 Februari 2024

Waziri wa mambo ya kigeni Ujerumani Annalena Baerbock amesema ni jukumu la Israel kuhakikisha kunakuwa na maeneo salama kwa raia wanaojihifadhi kwenye mji wa Rafah kabla ya kufanya operesheni yoyote ya kijeshi.

https://p.dw.com/p/4cM7w
Ujerumani | Ziara ya waziri wa mambo ya nje wa Poland mjini Berlin
Waziri wa mambo ya nje Ujerumani Annalena BaerbockPicha: Ebrahim Noroozi/AP Photo/picture alliance

Ametoa matamshi hayo wakati shinikizo la kimataifa linaongezeka dhidi ya serikali mjini Tel Aviv kuchukua hatua zote zinazohitajika kuepusha janga zaidi la kibinadamu kwenye mpango wake wa kuushambulia mji wa Rafah.

Zaidi kuhusu umuhimu wa kuwalinda raia wa mji huo bibi Baerbock amesema,

"Iwapo hivi sasa operesheni inafanyika dhidi ya kundi la kigaidi la (Hamas) huko Rafah, hilo ni jukumu letu la pamoja, lakini pia ni wajibu wa jeshi la Israel kutenga maeneo salama kwa watu waliotafuta hifadhi, na sehemu wanayoweza kwenda kwa usalama," alisema Baerbock.

Marekani na Umoja wa Mataifa tayari zimekwishaionya Israel kutoushambulia mji wa Rafah bila ya kuwa na mpango madhubuti wa kuwalinda raia, ambao inaarifiwa hawana mahala pengine pa kwenda.