1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Al- Sisi aukaribia urais Misri

27 Mei 2014

Mkuu wa majeshi wa zamani nchini Misri Abdel Fattah al-Sisi anatarajiwa kuibuka mshindi katika siku ya pili ya uchaguzi wa rais nchini humo na kuurudisha wadhifa huo wa urais kwenye mikono ya mwanajeshi.

https://p.dw.com/p/1C7Ve
Abdel Fatah al-Sisi mkuu wa majeshi wa zamani na mgombea urais nchini Misri.
Abdel Fatah al-Sisi mkuu wa majeshi wa zamani na mgombea urais nchini Misri.Picha: Reuters

Al- Sisi mwenye umri wa miaka 59 alikuwa anataraji kujitokeza kwa idadi kubwa ya watu kupiga kura zao kutapeleka ujumbe kwa mataifa ya magharibi kwamba kumuondowa kwake madarakani takriban mwaka mmoja uliopita Mohamed Mursi rais wa itikadi kali za Kiislam aliechaguliwa kwa njia ya kidemokrasia hayakuwa mapinduzi ya kijeshi bali ni mapinduzi ya umma kama yale yaliyokomesha utawala wa kidikteta wa miaka thelathini wa Hosni Mubarak.

Katika juhudi za kushaiijisha watu kuzidi kujitokeza kupiga kura zao serikali imetangaza leo kuwa ni siku ya mapumziko na kuongeza muda wa kupia kura kwa saa moja zaidi ambapo vituo vya kupiga kura sasa vitafungwa saa nne usiku.

Wakati ushindi wa Sisi tayari ni jambo linalojulikana kujitokeza kwa idadi kubwa ya wapiga kura kunaonekana kuwa ni muhimu kumpa uhalali Jemedari huyo Mkuu aliyempinduwa rais wa kwanza aliechaguliwa kidemokrasia nchini Misri Mohamed Mursi wa chama cha Udugu wa Kiislamu.

Idadi ndogo ya wapiga kura

Kujitokeza kwa idadi ndogo ya wapiga kura ni tafauti kabisa na hali ilivyokuwa wakati wa uchaguzi wa rais na bunge uliofanyika baada ya kupinduliwa kwa Mubarak ambapo wapiga kura kwa mamia walikuwa kwenye misururu mirefu kuelekea vituo vya kupiga kura.Sehemu kubwa ya watu walijitokeza kupiga kura zaio hapo jana ilikuwa ni ile ya kizazi cha wazee.

Wapiga kura Cairo.
Wapiga kura Cairo.Picha: Reuters

Katika ngome kuu za chama cha Udugu wa Kiislamu na washirika wao wa itikadi kali za Kiislamu ambao walikuwa wakihodhi chaguzi nyengine zote tokea kupinduliwa kwa Mubarak kulikuwa takriban hakuna kabisa zoezi hilo la uchaguzi baada ya kundi hilo kutowa wito wa kuususia.

Hatua yao hiyo imepunguza idadi kubwa ya watu milioni 54 waliojiandikisha kupiga kura kushiriki uchaguzi huo.

Sisi muokozi pekee

Kwa miezi kumi tokea kupinduliwa kwa Mursi na jeshi wakati huo likiongozwa na al - Sisi ,mkuu huyo wa zamani wa majeshi alikuwa akiungwa mkono takriban na taasisi zote za serikali na vyombo vya habari vikimwelezea kuwa ni mtu pekee wa kuikowa nchi hiyo.

Wafuasi wa al- Sisi Cairo.
Wafuasi wa al- Sisi Cairo.Picha: DW/Mostafa Hashem

Mpinzani wake pekee katika kinyan'ganyiro hicho ni Hamdeen Sabahi mwanasiasa wa mrengo wa shoto aliyemalizia nafasi ya tatu katika uchaguzi wa rais wa mwaka 2012 ambaye inaaminika kuwa hawezi kupata kura nyingi.

Mandishi : Mohamed Dahman/Reuters/AP

Mhariri: Josephat Charo