1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Operesheni kupambana na waasi yaanza Ukraine

15 Aprili 2014

Operesheni iliokuwa ikisubiriwa kwa muda mrefu ya kuwan'gowa wanaharakati wanaotaka kujitenga mashariki mwa Ukraine imeanza wakati Urusi ikitupilia mbali madai kwamba imeweka vikosi vyake katika eneo hilo.

https://p.dw.com/p/1BjCl
Wanajeshi wa Ukraine wakiwa pembeni ya helikopta ya kivita na gari la deraya katika kituo cha ukaguzi karibu na mji Izium mashariki ya Ukrainei.(15.04.2014)
Wanajeshi wa Ukraine wakiwa pembeni ya helikopta ya kivita na gari la deraya katika kituo cha ukaguzi karibu na mji Izium mashariki ya Ukraine.(15.04.2014)Picha: REUTERS

Rais wa Ukraine Oleksandr Turchynov ameliambia bunge leo hii kwamba vikosi vya nchi hiyo vinawekwa kaskazini ya mji wa Donetsk karibu na mpaka na Urusi.Rais huyo hakutowa maelezo ya kina isipokuwa tu amesema operesheni hiyo itafanyika kwa njia ya kuwajibika na kwa kuzingatia uwiano. Turychnov amewaambia wabunge kwamba lengo ni kuwalinda raia dhidi ya magaidi wanaojaribu kuigawa vipande vipande nchi hiyo.

Waasi wanaodai kupatiwa mamlaka makubwa zaidi ya kujiamuliwa mambo yao kutoka serikali ya Ukraine na kuwa na uhusiano wa karibu na Urusi wameendelea kuyakalia majengo ya serikali ikiwemo polisi katika miji ya mashariki licha ya kumalizika kwa muda wa mwisho uliowataka kusalimisha silaha zao hapo jana.

Waasi kuangamizwa

Generali wa Ukraine anayeongoza operesheni hiyo mashariki mwa Ukraine ameonya kwamba wanaharakati wanaogoma kuweka chini silaha zao wataangamizwa.

Wanajeshi wa Ukraine wakiwa pembeni ya helikopta ya kivita na gari la deraya katika kituo cha ukaguzi karibu na mji Izium mashariki ya Ukraoi.(15.04.2014)
Wanajeshi wa Ukraine katika kituo cha ukaguzi karibu na mji Izium mashariki ya Ukraine. (15.04.2014)Picha: REUTERS

Generali Valeriy Krutov wa Shirika la Usalama la Ukraine (SBU) amewaambia waandishi wa habari leo hii watu hao lazima waonywe kwamba iwapo hawatosalimisha silaha zao wataangamizwa na kuongeza kwamba wanamgambo hao wanasaidiwa na mamia ya wanajeshi kutoka Kurugenzi Kuu ya Ujasusi ya Urusi(GRU).

Hata hivyo Dmitry Peskov msemaji wa Rais Vladimir Putin wa Urusi amesema leo hii kwamba hakuna vikosi vya kijeshi vya Urusi mashariki ya Ukraine na kwamba madai yoyote ya kuwepo kwao huko ni upuuzi.

Amesema kwamba serikali za mataifa ya magharibi kwa makusudi zimekuwa zikipuuza hakikisho juu ya suala hilo kutoka Urusi na kwamba kinachowashangaza ni kuamuwa kutosikiliza taarifa zozozote kutoka upande wa Urusi.

Hofu ya vita va wenyewe kwa wenyewe

Naye Waziri Mkuu wa Urusi Dmitry Medvedev ametowa picha ya kutisha baada ya watu wawili kuuwawa hapo Jumapili wakati serikali ya Ukraine ilipojaribu bila ya mafanikio kuudhibiti tena mji wa Slaviansk ulioko kama kilomita 150 kutoka mpaka wa Urusi.

Wanaharakati wanaotaka kujitenga wakiwa katika mji wa Gorlivka mashariki ya Ukraine ambapo wamekiteka kituo cha polisi cha wilaya. (15.04.2014)
Wanaharakati wanaotaka kujitenga wakiwa katika mji wa Gorlivka mashariki ya Ukraine ambapo wamekiteka kituo cha polisi cha wilaya. (15.04.2014)Picha: picture alliance/AA

Amesema kwenye mtandao wake wa Facebook kwamba nchi hiyo iko kwenye ukingo wa vita vya wenyewe kwa wenyewe.

Naye Seneta John McCain ameitaka serikali ya Marekani kuipatia silaha serikali ya Ukraine Akizungumza katika mji mkuu wa Estonia,Tallin amesema hawana hata zana za kujihami ambazo wanazihitaji mno na kwa wao kutofanya hivyo ni jambo lisilokubalika na aibu na kwamba yeye mwenyewe binafsi anaona karaha kwamba hawawapatii kile wanachohitaji kuilinda nchi yao.

Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Kujihami ya NATO Anders Fogh Rasmussen amesema leo Urusi inahusika sana na mzozo ulioko mashariki ya Ukraine.

Mwandishi: Mohamed Dahman/dpa/Reuters

Mhariri:Yusuf Saumu