1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Obama: Tulikadiria vibaya uwezo wa IS

Admin.WagnerD29 Septemba 2014

Rais wa Marekani Barack Obama amesema nchi yake ilikisia vibaya nguvu za kundi la IS, na uwezo wa jeshi la Irak kukabiliana na kundi hilo. Wakati huo huo mashambulizi yameendelea dhidi ya kundi hilo

https://p.dw.com/p/1DMYR
Rais wa Marekani Barack Obama amesema nchi yake iliubeza uwezo wa kundi la IS
Rais wa Marekani Barack Obama amesema nchi yake iliubeza uwezo wa kundi la ISPicha: Jim Watson/AFP/Getty Images

Mashambulizi ya anga yaliyofanywa usiku wa kuamkia leo dhidi ya kundi hilo lijulikanalo kama Dola la Kiislamu, au IS, yamejikita katika mikoa miwili ya Raqa na Aleppo ambayo ni ngome muhimu za kundi hilo, hii ikiwa ni kwa mujibu wa shirika la kuchunguza haki za binadamu nchini Syria ambalo lina makao yake makuu nchini Uingereza.

Shirika hilo limesema kwamba miongoni mwa vituo vilivyolengwa ni pamoja na kiwanda cha kusindika nafaka katika mji unaoshikiliwa na Is wa Minbej, ambacho kilikuwa kikiendeshwa na raia wa kawaida. Mkuu wa shirika hilo Rami Abdel Rahman amesema wanazo taarifa kuwa raia wameuawa katika shambulizi hilo, lakini hakuthibitisha idadi ya wahanga.

Shabaha nyingine ya mashambulizi ya usiku wa leo ilikuwa makao makuu ya kimkoa ya Dola la Kiislamu yaliyo kati ya mji wa Minbej na Jarabulus ambao uko kaskazini zaidi. Katika mkoa wa Raqa, ndege za Marekani na washirika wake zimeshambulia kizuizi cha barabarani, nje kidogo ya ya mji wa Raqa ambao ndio makao makuu ya kundi hilo.

Madege ya kivita ya Marekani na washirika wake yameendelea kuzipiga ngome za ´'Dola la Kiislamu''
Madege ya kivita ya Marekani na washirika wake yameendelea kuzipiga ngome za ´'Dola la Kiislamu''Picha: Reuters/ECPAD

Makadirio mabaya

Huku mashambulizi hayo yakiendelea, rais wa Marekani Barack Obama amesema kupitia mazungumzo na kituo kimoja cha televisheni nchini Marekani, kwamba walikuwa na makisio yasiyo sahihi kuhusu uwezo wa kundi hilo.

''Mkuu wa taasisi zetu za ujasusi Jim Clapper ameekiri kwamba makadirio yao juu ya kile kinachofanyika nchini Syria yalikuwa ya chini.'' Amesema Obama.

Obama alisema kuwa wapiganaji wa kijihadi waliofurushwa kutoka Irak kabla ya majeshi ya Marekani kuondoka mwaka 2011, wote walihamia nchini Syria, na kwamba kwa msaada wa makabila ya madhehebu ya Suni wameweza kujikusanya na kuunda kundi hatari zaidi la IS.

Uwezo wa jeshi la Irak

Hali kadhalika rais Obama alikiri katika mazungumzo hayo na kituo cha Televisheni, kuwa Marekana ilijidanganya kwa makadirio ya uwezo wa Irak kukabiliana na kundi hilo.

Wapiganaji wa IS wanashikilia maeneo makubwa nchini Irak na Syria
Wapiganaji wa IS wanashikilia maeneo makubwa nchini Irak na SyriaPicha: picture-alliance/abaca/Yaghobzadeh Rafael

Maeneo mengine yalipigwa katika mashambulizi ya jana ni pamoja na mji wa Tal Abyad ulio karibu na mpaka baina ya Syria na Uturuki, ambako shule inayotumiwa kuwahifadhi wanamgambo imepigwa.

Kabla ya mashambulizi haya ya karibuni, ndege za washirika wa Marekani zililiharibu lango la mtambo mkubwa zaidi wa gesi nchini Syria mashariki mwa mji wa Deir Ezzor, katika kile kilichochukuliwa kama onyo kwa wanamgambo wa IS wanaokishikilia kuwataka wahame.

Mtambo huo huvihudumia vituo kadhaa vya umeme katika mkoa wa Homs unaodhibitiwa na serikali, na ikiwa kitaacha kufanya kazi mikoa kadhaa itabaki bila umeme.

Mwandishi: Daniel Gakuba/APE/RTRE/AFPE

Mhariri: Mohammed Khelef