1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mwanasiasa mashuhuri auwawa Urusi

28 Februari 2015

Boris Nemtsov kiongozi wa upinzani mwenye heba na mkosoaji mkubwa wa rais Vladimir Putin wa Urusi ameuwawa kwa kupigwa risasi karibu na Ikulu Moscow Ijumaa usiku. (27.02.2015).

https://p.dw.com/p/1Ej77
Boris Nemtsov mwanasiasa mashuhuri wa upinzani aliyeuwawa Urusi.
Boris Nemtsov mwanasiasa mashuhuri wa upinzani aliyeuwawa Urusi.Picha: AFP/Getty Images/A. Nemenov

Kifo chake kinakuja siku moja kabla ya maandamano yaliyopangwa kufanyika dhidi ya serikali hapo Jumapili ambapo alikuwa akitazamiwa kuhudhuria.

Kifo cha Nemtsov, mwenye umri wa miaka 55 naibu waziri mkuu wa zamani , kimezusha hasira miongoni mwa viongozi wa upinzani ambao wameishutumu serikali ya Urusi kwa kujenga hali ya kutovumilia upinzani wowote na kuyaita mauaji hayo ni ya kukusudia.

Rais Putin haraka alituma salamu zake za rambi rambi na kuyaita mauaji hayo kuwa ni ya uchokozi.

Nemtsov alikuwa akiandika ripoti ikitoa ushahidi kwamba anaamini unathibitisha kuhusika moja kwa moja kwa Urusi katika uasi wa wapiganaji wanaotaka kujitenga ambao umekuwa ukiendelea mashariki mwa Ukraine tangu Aprili mwaka jana.

Polisi wakiuchukuwa mwili wa marehemu Boris Nemtsov baada ya kupigwa risasi na kuuwawa mjini Moscow. (28.02.2015)
Polisi wakiuchukuwa mwili wa marehemu Boris Nemtsov baada ya kupigwa risasi na kuuwawa mjini Moscow. (28.02.2015)Picha: REUTERS/Maxim Shemetov

Ukraine na mataifa ya magharibi wanaishutumu Urusi kwa kuwaunga mkono waasi kwa kuwapatia wanajeshi na silaha za kisasa. Urusi inakana shutuma hizo.

Putin aamuru uchunguzi

Putin amewaamuru wakuu wanaohusika na ulinzi wa sheria nchini humo kuangalia juu ya uchunguzi katika kifo cha Nemtsov.

"Putin amedokeza kwamba mauaji haya ya kinyama yanaishara zote za mtu aliyekodiwa na yanaleta uchochezi," msemaji wa rais Dmitry Peskov amesema katika matamshi yaliyotangazwa na shirika la habari la Urusi.

Rais Barack Obama ameitaka serikali ya Urusi kufanya uchunguzi wa " haraka, usioelemea upande wowote na wa uwazi" na kuwafikisha wahusika katika vyombo vya sheria. Obama amemuita Nemtsov kuwa " mtetezi wa watu asiyechoka" kwa ajili ya haki za raia wa Urusi.

Watu wakiweka maua katika eneo alikouwawa Boris Nemtsov Moscow. (28.02.2015)
Watu wakiweka maua katika eneo alikouwawa Boris Nemtsov Moscow. (28.02.2015)Picha: REUTERS/Sergei Karpukhin

Waziri wa mambo ya kigeni wa Marekani John Kerry amesema Nemtsov amejitolea maisha yake kupigania demokrasia nchini Urusi, "na uhusiano imara kati ya Urusi na mataifa jirani pamoja na washirika, ikiwa ni pamoja na Marekani."

Nemtsov amekuwa akishutumu udhaifu wa serikali , rushwa iliyokithiri pamoja na sera za Urusi kuelekea Ukraine, ambazo zimesababisha kuharibika kwa uhusiano kati ya Urusi na mataifa ya magharibi kwa kiwango ambacho hakijawahi kuonekana tangu wakati wa vita baridi.

Hakuwa na woga

Katika mahojiano na gazeti la Sobesednik , Nemtsov amesema mapema mwezi huu kuwa mama yake mwenye umri wa miaka 86 anawasi wasi kwamba Putin anaweza kumuua kutokana na shughuli zake za upinzani. Alipoulizwa iwapo ana hofu kama hizo binafsi, alijibu kwa kusema : "Iwapo ningekuwa na hofu nisingeweza kuongoza chama cha upinzani."

Akizungumza katika radio saa chache kabla ya kifo chake, alimkosoa vikali rais Putin kwa kuitumbukiza Urusi katika mzozo kwa "ukichaa wa uvamizi na sera hatari za vita dhidi ya Ukraine."

Boris Nemtsov mwanasiasa mashuhuri wa upinzani aliyeuwawa Urusi.
Boris Nemtsov mwanasiasa mashuhuri wa upinzani aliyeuwawa Urusi.Picha: picture-alliance/dpa/M. Blinov

"Nchi inahitaji mageuzi ya kisiasa," Nemtosv amesema katika radio ya Ekho Moskvy. "Wakati madaraka yako katika mikono ya mtu mmoja tu na mtu huyu anatawala milele, hii itaelekeza katika maafa makubwa, makubwa kabisa.

Rais wa Ukraine Petro Poroshenko amemuita Nemtsov kuwa ni mtu rafiki na "daraja" kati ya nchi hizo mbili. Amesema katika ukurasa wa Facebook kwamba anamatumaini wauwaji wataadhibiwa.

Mwandishi: Sekione Kitojo / ape

Mhariri : Mohamed Dahman