1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mtoto wa kike ahitimu shule

20 Aprili 2011

Kutojua kusoma na kuandika ni jambo ambalo linaweza kukuaibisha na linayaathiri maendeleo ya mtu binafsi.Hilo ndilo wanalolitambua ndugu wawili Latifa na Elinam katika makala haya mapya ya Noa Bongo-Jenga Maisha Yako.

https://p.dw.com/p/OaLF
Msichana akiwa shuleniPicha: LAIF

Kujua kusoma na kuandika pamoja na elimu ni mambo muhimu yanayokubalika kuwa chachu ya maendeleo. Hata hivyo, kiasi cha zaidi ya watu wazima milioni 150 kote ulimwenguni hawawezi kusoma na kuandika. Mwaka 2003 Shirika la Umoja wa Mataifa lilizindua rasmi muongo wa kuzipa msukumo harakati za kuiongeza idadi ya watu wanaoweza kusoma na kuandika ifikapo mwaka 2012. Elimu pia ni moja ya malengo ya milenia ya maendeleo ya Umoja wa Mataifa.

Watoto wa kike wana uwezekano mkubwa zaidi wa kutopata elimu na wengi wao hulazimika kuacha shule mapema pale wazazi wanaposhindwa kuwalipia karo wana wao wote ili waende shule kila wakati.

Katika mchezo huu, Latifa anakabiliwa na tatizo hilo ijapokuwa amekuwa akipata alama nzuri shuleni. Biashara ya Papa Wali imevurugika - jambo linalomlazimu Latifa kuchangia katika shughuli za kila siku za kuyakimu mahitaji ya familia. Wazazi wake Latifa nao hawajui kusoma na kuandika na wanalazimika kuzitathmini athari za kutomsomesha binti yao. Jee, mchango na ushawishi wa kakake Elinam na rafikiye Zakia utaweza kuwa chachu ya mabadiliko? Ipi hatima ya Epiphane, mfanyakazi wa Papa Wali asiyejua kusoma na kuandika?

Michezo ya Noa Bongo: Jenga Maisha Yako inaweza kusikilizwa katika lugha sita tofauti: Kiswahili, Kiingereza, Kifaransa, Kihausa, Kireno na Kihabeshi. Mradi huu unaungwa mkono na Wizara ya Mambo ya Nje ya Ujerumani.