1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mipango ya kupunguza polisi katika Bundesliga

15 Agosti 2014

Baada ya Bremen, jimbo jingine limetangaza mipango hiyo tena: maafisa wa North Rhine Westphalia wamechoka kuwalipa polisi wa ziada wa kupambana na ghasia katika mechi za Bundesliga

https://p.dw.com/p/1CvXv
Fußball Derby Fans Borussia Dortmund FC Schalke 04
Picha: picture-alliance/dpa

Huku ikiwa nimesalia chini ya wiki moja tu kabla ya msimu wa 2014/2015 kuanza, mambo yanaendelea kutokota kuhusiana na suala la usalama wa viwanjani. Katika mji wa kaskazini wa Bremen, maafisa wametangaza kuwa kampuni inayohusika na ligi kuu ya Ujerumani, DFL – Deutsche Fußball Liga GmbH, itaanza kuwalipa polisi ambao watatumika katika mechi za ligi.

Na sasa jimbo la North Rhine Westphalia NRW limetangaza kuwa polisi wa eneo hilo watapunguzwa katika viwanja vya michezo. Au katika baadhi ya matukio hawatahitajika kabisa katika mechi za Bundesliga za eneo hilo kuanzia msimu huu. Jimbohilo ni mojawapo ya maeneo ya vilabu vingi vya Bundesliga: ni nyumbani kwa timu sita za Bundesliga – Dortmund, Schalke, Cologne, Leverkusen, Borussia Moenchengladbach na Paderborn.

Fußball Bundesliga 12. Spieltag Hannover 96 gegen Eintracht Braunschweig
Katika siku za usoni mashabiki hawatasindikizwa viwanjani na polisiPicha: picture-alliance/dpa

Kwa mujibu wa mipango iliyotangazwa waziri wa mambo ya ndani Ralf Jäger, polisi watawekwa “katika maeneo yaliyofichika na pia watatumika kwa kiwango kidogo sana kuyasindikiza makundi ya mashabiki”.

Hii ni kutokana na gharama kubwa zinazotolewa kwa polisi wanaotoa ulinzi katika mechi za Bundesliga. Sasa mashabiki wanaombwa kuwajibika wenyewe. Kama hilo litafanikiwa au la, tutaweza kuona wakati mechi za ligi zitakapoanza wiki ijayo..

Hata hivyo hatua hiyo ya Kupunguzwa polisi katika mechi za Bundelsiga haichukuliwi katika miji yote ya Ujerumani. Berlin kwa mfano imethibitisha kuwa haitajihusisha na mpango huo wa majaribio kwa wakati huu.

Katika ligi nyingine kuu za Ulaya, kwa miaka mingi vilabu hutakiwa kugharamia malipo ya polisi wanaotoa ulinzi. Vilabu vya Ufaransa kwa mfano, hulipa sehemu ya gharama za malipo ya polisi wakati wa siku ya mchuano. Katika ligi ya Uhispania Primera Division na Premier League ya England, serikali huwalipa polisi wanaoweka ulinzi nje ya wiwanja pekee. Nchini Uhispania, vilabu hasa hutumia kampuni za kibinafsi za usalama, ndani ya viwanja ili kuwathibiti mashabiki. Nchini England, ni jukumu la vilabu kuhakikisha usalama wa ndani ya viwanja vyao.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/DPA/AP
Mhariri: Yusuf Saumu