1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Koffi Annan:Itakuwa fedheha kwa Afrika kujiondoa ICC

Admin.WagnerD8 Oktoba 2013

Katibu mkuu wa zamani wa umoja wa Mataifa Koffi Annan amesema itakuwa 'alama ya aibu' kwa bara Afrika iwapo itajiondoa kutoka mkataba wa Roma uliounda mahakama ya kimataifa inayoshughulikia kesi za uhalifu ICC

https://p.dw.com/p/19w0p
Makao makuu ya ICC mjini The Hague
Makao makuu ya ICC mjini The HaguePicha: Getty Images

Akizungumza mjini Cape Town nchini Afrika kusini,Annan alisema ni viongozi wachache wanaoipinga na kuipiga vita ICC na kuonya dhidi ya kujiondoa katika mahakama hiyo ya kimataifa bila ya kuwa na mfumo mwingine wa sheria mbadala.

Kiongozi huyo wa zamani wa umoja wa Mataifa amesema ikiwa viongozi wa Afrika wataipiga vita ICC,na kujiondoa itakuwa fedheha kubwa kwa kila mmoja wao na nchi zao na kukanusha kuwa ICC ina dhamira ya kuwaandama viongozi wa kiafrika na badala yake kuwashutumu viongozi hao kwa kulinda masilahi yao ya kibinafsi na sio ya waafrika wote.

Katibu mkuu wa zamani wa Umoja wa Mataifa Koffi Annan
Katibu mkuu wa zamani wa Umoja wa Mataifa Koffi AnnanPicha: AP

Kujiondoa kwaonyesha kutoheshimu sheria

Akitoa mhadhara unaofanyika kila mwaka wa wakfu wa Desmond Tutu kuadhimisha miaka 82 tangu kuzaliwa kwa mshindi huyo wa tuzo ya amani ya Nobel,Annan amesisitiza kuwa njama ya kutaka kujiondoa kwa nchi za Afrika kutoka mahakama hiyo ya ICC ni ishara dhahiri kuwa kuna desturi ya kutoheshimu sheria na watuhumiwa wanaokabiliwa na mashitaka katika mahakama hiyo wamefikishwa ICC kama watu binafsi na sio bara Afrika.

Huku kampeini za kuipinga mahakama hiyo ya ICC zikipamba moto,umoja wa Afrika AU unatarajiwa kufanya kikao maalum kati ya Ijumma na Jumamosi hii kujadili uhusiano wa nchi za Afrika na mahakama hiyo inayoshughulikia kesi za mauaji ya halaiki,uhalifu wa kivita na uhalifu dhidi ya binadamu.

AU kujadili kujiondoa kwa Afrika ICC

Mkutano huo unafuatia shutuma kutoka umoja huo wa Afrika unaoshirikisha nchi 54 wanachama kuwa ICC inawalenga hususan waafrika katika mashitaka yao wakitaja kesi za watu mashuhuri kama aliyekuwa rais wa Liberia Charles Taylor,Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta na naibu wake William Ruto.

Viongozi wa Afrika mjini Addis Ababa
Viongozi wa Afrika mjini Addis AbabaPicha: Reuters

Annan anahoji ICC ilikuwa kimbilio la mwisho kwa nchi zisizo na mfumo dhabiti wa idara ya mahakama lakini kufuatia yanayojiri hivi karibuni, ni bayana viongozi wanajilinda wenyewe kwa wenyewe huku waathiriwa wakikosa wa kuwatetea.

Kesi nne miongoni mwa niyngine mbele ya mahakama hiyo ya ICC ziliwasilishwa na viongozi wa kiafrika wenyewe ilhali baraza la usalama la umoja wa Mataifa limewasilisha nyingine mbili zinazoihusu Darfur na Libya

Kesi dhidi ya naibu rais wa Kenya Ruto ilianza mwezi uliopita na kesi dhidi ya Rais wa nchi hiyo inatarajiwa kuanza mwezi Novemba.Wote wawili wanashitakiwa kwa kuhusika katika ghasia za baada ya uchaguzi wa mwaka 2007.

AU imeitaka ICC kutupilia mbali kesi dhidi ya viongozi hao wawili wa Kenya huku wabunge wa nchi hiyo wakiwa wamepiga kura kutaka kujiondoa kutoka mkataba wa Roma.

Nchi 34 za Afrika ni miongoni mwa nchi 122 wanachama wa mkataba huo wa Roma uliounda mahakama hiyo ya kimataifa iliyoanza kufanya kazi tarehe 1 mwezi Julai mwaka 2002.

Mwandishi:Caro Robi/afp

Mhariri: Yusuf Saumu