1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jordan yataka kuwepo ustahimilivu kati ya Israel na Palestina

Admin.WagnerD19 Novemba 2014

Jordan leo imetaka kuwepo ustahamilivu na utulivu mjini Jerusalem baada ya wapalestina wawili kuwaua watu watano katika sinagogi la wayahudi hapo jana na kuichochea Israel kuanza kubomoa nyumba za washambualiaji

https://p.dw.com/p/1Dq0L
Picha: Reuters/R. Zvulun

Jordan ambayo ndiyo msimamizi wa eneo takatifu la mashariki mwa Jerusalem ambako kuna msikiti wa Al Aqsa ambao umesababisha mzozo wa hivi karibuni kati ya waislamu wa kipalestina na wayahudi wa Israel pia imeitaka Israel kusitisha vitendo ambavyo huenda vikachochea uhasama zaidi katika eneo hilo takatifu linalogombaniwa.

Msemaji wa serikali ya Jordan Mohammed Mumeni amesema nchi yake inalaani vitendo vyote vya ghasia na kigaidi vinavyowalenga raia bila ya kujali vinatokea upande upi na kwa dhamira ipi na kuongeza serikali ya Jordan inafuatilia kwa karibu hali ilivyo Jerusalem.

Waziri mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu kwa mara nyingine ametoa hakikisho kuwa nchi yake haina mipango ya kukiuka makubaliano kuhusu hadhi ya eneo takatifu la mashariki mwa Jerusalem kuliko msikiti wa Al Aqsa.

Papa aomba amani mashariki ya kati

Kiongozi wa kanisa Katoliki Papa Francis pia amelaani shambulizi la jana katika sinagogi na kuzitaka Israel na Palestina kuchukua hatu za kijasiri kuhakikisha kunapatikana amani kati yao.

Kiongozi wa kanisa Katoliki Duniani Papa Francis
Kiongozi wa kanisa Katoliki Duniani Papa FrancisPicha: AFP/Getty Images/F. Monteforte

Israel leo imeanzisha tena sera ambayo ilisitishwa mwaka 2005 ya kuzibomoa nyumba za washambuliaji wanaowalenga kwa kuyabomoa makaazi ya familia ya kijana wa kipalestina aliyeuawa mwezi uliopita baada ya kuwauwa watu watatu waliokuwa wakisubiri kuabiri treni mjini Jerusalem kwa kuwagonga kwa gari lake.

Makaazi mengine matatu ya familia za wapalestina waliowashambulia waisrael katika kipindi cha hivi karibuni pia yamepangiwa kubomolewa. Mashirika ya kutetea haki za binadamu yamelaani hatua hiyo ya Israel kwa kusema inakiuka haki za kimataifa kwa kuwalenga jamaa za washambuliaji ambao hawana hatia.

Israel yakosoa juhudi za kutambuliwa kwa Palestina

Wakati huo huo, Israel imeitaja hatua ya wabunge wa Uhispania kupiga kura hapo jana kuitambua Palestina kama taifa huru kuwa kitendo kisichosaidia.Taarifa kutoka wizara ya mambo ya nje ya Israel imesema hatua hiyo ya wabunge wa Uhispania inafanya hata matumaini ya kufikiwa amani kati ya Israel na Palestina kuwa ndoto kwani inawahimiza wapalestina kuwa na misimamo mikali.

Waziri mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu
Waziri mkuu wa Israel Benjamin NetanyahuPicha: Reuters/Abir Sultan

Bunge la Ufaransa pia linatarajiwa kuunga mkono wito huo wa kuitaka serikali kuitambua Palestina kama taifa huru wakati wabunge watakapopiga kura tarehe 30 mwezi huu. Serikali ya Sweden mwezi uliopita iliitambua rasmi Palestina kama taifa huru na kusema huo utakuwa mwanzo wa kupatikana suluhisho la kudumu katika mzozo wa muda mrefu wa mashariki ya kati.

Netanyahu ameishutumu Jumuiya ya kimataifa kwa kupuuza umwagaji damu unaofanyika Israel na badala yake kutafuta kile alichokiita kuipa tuzo Palestina kwa kutaka liwe taifa huru na kusema hawataruhusu hilo lifanyike.

Mwandishi:Caro Robi/Afp/Ap

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman