1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Israel na Hamas waendelea na mapigano

Elizabeth Shoo20 Agosti 2014

Mgogoro kati ya Israel na Palestina unaendelea. Pande zote mbili zimekuwa zikishambuliana kwa maroketi. Wakati huo huo, Misri inataka mazungumzo ya kuleta amani yaanze tena.

https://p.dw.com/p/1CxP7
Ukanda wa Gaza ukishambuliwa na maroketi
Picha: REUTERS

Hali ya wasiwasi imerejea tena kwa wakaazi wa Israel na ukanda wa Gaza. Awali Israel na Hamas walikubaliana kuendeleza muda wa kusitisha mapigano. Lakini makubaliano hayo hayakuheshimiwa. Israel inasema kuwa hapo jana Hamas ilianza kurusha maroketi kuelekea Israel na ndipo Israel ilipojibu mashambulizi.

Wizara ya afya ya Palestina inaripoti vifo vya Wapalestina wasiopungua 10. Wengine 68 wamejeruhiwa. Israel kwa upande wake inasema kuwa ilifanya mashambulizi 60 ya angani. Ni mashambulizi yanayolenga nyumba za viongozi wa Hamas. Lakini sehemu kubwa ya watu wanaokufa ni raia wa kawaida. Bwana mmoja aliyeshuhudia mashambulizi kwa macho anaelezea kusikitishwa kwake na mauaji yanayoendelea. "Familia nzima imeuwawa: Baba, mke wake aliyekuwa na mimba pamoja na watoto wao watatu. Waisraeli wamelenga familia nzima bila kutoa taarifa na bila sababu yoyote."

Israel yalenga viongozi wa Hamas

Katika kisa kingine, watu watatu waliuwawa baada ya nyumba yao kubomolewa na roketi katika ukanda wa Gaza. Nyumba hiyo inaaminiwa kuwa ya kiongozi wa kijeshi wa Hamas, Mohammed Deif. Msemaji mmoja wa Hamas amethibitisha kuwa miongoni mwa waliouwawa walikuwepo mke na mtoto wa Deif. Waziri mmoja wa Israel amenukuliwa akisema kuwa Mohammed Deif anastahili kufa kama vile Osama bin Laden alivyokufa. Waziri huyo aliongezea kuwa Deif ni muuaji na kwamba Israel itatumia kila nafasi itakayojitokeza kujaribu kumuua kiongozi huyo wa Hamas.

Mgogoro kati ya Israel na Palestina unaendelea. Pande zote mbili zimekuwa zikishambuliana kwa maroketi. Wakati huo huo, Misri inataka mazungumzo ya kuleta amani yaanze tena.
Msikiti uliopo katika ukanda wa Gaza ulibomolewa na maroketi ya IsraelPicha: Reuters

Kwa sasa hakuna ishara za mgogoro huu kutulia. Israel imewaandaa maaskari 2,000 wa ziada kwa ajili ya kufanya operesheni za ardhini wakati wowote ule.

Hata mazungumzo ya kuleta amani yaliyokuwa yakiendelea Cairo, Misri yamesitishwa. Wawakilishi wa pande zote mbili wamegoma kuendelea na juhudi za kupata suluhu ya mgogoro. Misri imewaasa Hamas na Israel kurejea katika meza ya mazungumzo, ikisema kuwa inajaribu kushawishi pande zote mbili kuheshimu makubaliano ya kusitisha mapigano kwa muda. Kwa mujibu wa viongozi wa Palestina na wawakilishi wa Umoja wa Mataifa, zaidi ya watu 2,000 wameuwawa tangu mgogoro huu ulipoanza mwezi uliopita.

Mwandishi: Elizabeth Shoo/ap/afp

Mhariri: Saumu Yusuf