1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

IS yazidi kupigana licha ya mashambulizi dhidi yake

Admin.WagnerD28 Oktoba 2014

Ushirika unaoongozwa na Marekani umeendeleza mashambulizi ya anga dhidi ya kundi la IS ndani ya Syria na Irak, huku ushirika huo ukinuia kulipiga vita kundi hilo kupitia mtandao wa Intaneti linaoutumia kuvutia wafuasi.

https://p.dw.com/p/1Dd83
Marekani na washirika wake tayari wamefanya mashambulizi 6,600 dhidi ya kundi la IS.
Marekani na washirika wake tayari wamefanya mashambulizi 6,600 dhidi ya kundi la IS.Picha: Reuters/Kai Pfaffenbach

Maafisa wa jeshi la Marekani wamesema kuwa wamefanya mashambulizi saba ya anga dhidi ya kundi la IS kati ya Jumapili na jana Jumatatu. Mashambulizi hayo yalijikita nchini Irak, yakilenga ngome za kundi hilo karibu na bwawa la Mosul na katika maeneo ya mji Fallujah ulio kusini mashariki.

Msemaji wa wizara ya ulinzi ya Marekani Bill Urban amesema mashambulizi haya dhidi ya IS ambayo yalianza Agosti mwaka huu yameigharibu nchi hiyo kitita cha dola milioni 580. Kwa ujumla ndege za Marekani na za washirika wake zimefanya mashambulizi 6,600 dhidi ya IS.

Awali wizara ya ulinzi ya Marekani ilikuwa imesema mashambulizi hayo yanaigharimu dola milioni 7 kwa siku, lakini wachambuzi wa kujitegemea wamesema makadirio hayo ni ya chini.

Mkutano kuhusu wakimbizi wa Syria

Wakati hayo yakijiri Mashariki ya Kati, katika mji mkuu wa Ujerumani- Berlin leo umeanza mkutano wa kuzungumzia suala la wakimbizi wa vita vinavyoendelea nchini Syria. Wawakilishi wa nchi 40 zinazoshiriki katika mkutano huo, wanatafuta jibu kwa changamoto zitokanazo na upungufu wa msaada wa kibinadamu kuwasaidia wahanga wa vita hivyo.

Waziri wa Mambo ya nchi za nje wa Ujerumani Frank-Walter Steinmeier akiwa na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Nchi za Kiarabu Nabil Elaraby mjini Berlin
Waziri wa Mambo ya nchi za nje wa Ujerumani Frank-Walter Steinmeier akiwa na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Nchi za Kiarabu Nabil Elaraby mjini BerlinPicha: Reuters/Hannibal

Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Ujerumani Frank-Walter Steinmeier amesema kinachohitajika ni kuimarisha mkakati uliopo.

‘‘Hatuna haja ya kubadilisha mtazamo, bali kuimarisha mikakati iliyopo. Hatupaswi tu kuishia katika kuwashughulikia wakimbizi, tunalazimika pia kujihusisha na utangamano wa nchi zinazowapokea wakimbizi hao‘‘. Amesema Steinmeier.

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuwashughulikia wakimbizi UNHCR linakadiria kuwa watu milioni 3 wamekimbia kutoka Syria na kuhamia mataifa jirani, huku wengine zaidi ya milioni 6.5 wakiwa wakimbizi wa ndani ya nchi.

Majira ya baridi kali yanayokaribia ni kitisho kwa wakimbizi kutoka Syria
Majira ya baridi kali yanayokaribia ni kitisho kwa wakimbizi kutoka SyriaPicha: Reuters/Murad Sezer

Hakuna msaada kwa wakurdi wa Syria

Nchini Syria kwenyewe mapigano makali yameendelea karibu na mji muhimu wa Kobane ulio karibu na mpaka kati ya Syria na Uturuki. Mwandishi wa shirika la AFP aliye karibu na mji huo amesema wapiganaji wa kikurdi wamekuwa wakipigana kufa na kupona kuwazuia wanamgambo wa IS kusonga mbele wakiukaribia mji huo.

Bado hakuna dalili zozote za msaada ulioahidiwa kwa wakurdi hao; ahadi kwamba wanajeshi wa mamlaka ya wakurdi wa Irak wajulikanao kama Peshmerga wangewasili na zana nziti za kijeshi kuwasaidia wenzao wa Syria bado haijatimizwa. Afisa wa kikurdi amesema msaada huo umekwamishwa na Uturuki, ambayo ilikuwa imekubali kuwapa njia wanajeshi hao.

Mwandishi: Daniel Gakuba/AFPE/ DW website

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman