Rais Barack Obama wa Marekani ametangaza jimbo la Oklahoma kuwa eneo la maafa makubwa baada ya kimbunga kulipiga jimbo hilo hapo Jumapili na Jumatatu.
Obama pia ameamuru kutolewa kwa msaada wa serikali kusaidia juhudi za taifa na serikali ya mitaa kulisaidia jimbo hilo kurudi katika hali yake ya kawaida.Takriban watu 51 wameuwawa hapo jana wakati kimbunga hicho kilipopiga eneo la maili moja katika viunga vya mji wa Oklahoma na kuangamiza kabisa vitongoji viliopo pamoja na kusababisha moto.Upepo mkali wa kasi ya kilomita 320 kwa saa ulisomba hewani magari na magari makubwa ya mizigo na kuvunja majengo mengi.Inaripotiwa kuwa watu waliojitolea katika shughuli zua uokozi wamewatowa watoto kwenye vifusi vya jengo la shule wakati juhudi za kuwaokowa manusura zikiendelea. Eneo hilo hilo liliathiriwa na kimbunga hapo mwaka 1999.Idadi ya vifo inaweza kuongozeka na kupindukia 90.
U
Jeshi la Syria limedai kuliharibu gari moja la kijeshi la Israel ambalo lilivuka mpaka katika eneo la milima ya Golan. Jeshi lilitangaza katika taarifa kwa njia ya televisheni iliosema kwamba gari hilo liliharibiwa pamoja na kila kitu kilichokuwemo ndani. Imesema lilivuka eneo la usimamishaji mapigano na lilikuwa likielekea kijiji cha Bir Ajam katika sehemu ya Syria iliokombolewa kwenye milima ya Golan.Jeshi la Israel halikusema lolote juu ya tukio hilo na iwapo gari lake liliharibiwa.
Rais Hamid Karzai wa Afghanistan ataomba msaada zaidi wa kijeshi wakati wa mazungumuzo yake na viongozi wa India leo hii katika juhudi za kuimarisha vikosi vyake vya usalama baada ya vikosi vya kimataifa kuondoka nchini humo hapo mwakani.
Katika ziara yake nchini India Karzai anatazamiwa kuwa na mazungumzo baadae leo hii na Waziri Mkuu Manmohan Singh na rais mwenzake wa India Pranab Mukherjee baada ya kupokea shahada ya heshima hapo jana usiku katika chuo kikuu cha jimbo la kaskazini la Punjab.Kiongozi huyo wa Afghanistan aliushukuru India kwa kuiunga mkono Afghanistan tokea aingie madarakani hapo mwaka 2001 baada ya kuanguka kwa utawala wa Taliban Kwa mujibu wa shirika la habari la Press Trust of India Karzai amesema India ikiwa kama rafiki wa Afghanistan imetowa mchango mkubwa sana katika kuinuwa maisha ya vijana wa Afghanistan.
Vikosi vya polisi vimeendelea kuzikalia kwa siku ya pili mfululizo ofisi za vyombo mashuhuri vya habari nchini humo huku kukiwa na wasi wasi kwamba kuna mkono wa kisiasa katika hatua hiyo unaomhusisha rais wa nchi hiyo.Ofisi za gazeti la Daily Monitor,the Observer na jarida la Red Paper pamoja na vituo viwili vya radio ambavyo vinamilikiwa na kampuni ya habari ya Nation Media Group zimezingirwa na polisi.Shirika la Haki za Binaadamu la Human Rights Watch lenye makao yake makuu mjini New York Marekani limesema serikali ya Uganda inapaswa kukomesha mara moja vitisho vya polisi vinavyochochewa kisiasa kwa magazeti na vituo vya radio na kuhakikisha kwamba vyombo vya habari vinafanya kazi vikiwa huru.
Polisi imesema kwamba wamepewa amri ya kuzipekuwa ofisi za kampuni hiyo ya habari kwa ajili ya kupata nyaraka zenye kuthibitisha kwamba Generali wa kijeshi David Sejusa amesema kwamba Brigedia Muhoozi Kainerugaba mtoto wa kiume wa Rais Yoweri Museveni anaandaliwa kuwa rais wa nchi hiyo.
Rais Barack Obama wa Marekani atafanya ziara ya kwanza barani Afrika mwezi ujao ambapo atazitembelea Senegal, Tanzania na Afrika Kusini. Hata hivyo ratiba iliotolewa imeonyesha hatoizuru Kenya nchi yake ya asili. Kiongozi huyo anadhamira ya kushajiisha mageuzi makubwa katika kanda hiyo kwa kulipa kipa umbele suala la demokrasia na mageizi ya kiuchumi. Ikulu mjini Washington ilisema ziara hiyo iliokuwa ikisubiriwa kwa muda mrefu inakusudia kuimarisha ushirikiano wa Marekani na watu wa kusini mwa jangwa la Sahara barani Afrika, ili kuendeleza amani na maendeleo. Wakati wa ziara hiyo, Obama atakutana na maafisa wa nchi husika, wafanyabiashara na viongozi wa jumuiya za kiraia wakiwemo vijana. Ziara yake itafanyika kati ya Juni 26 na Julai 3.
Mahakama Kuu ya Guatemala imetengua hukumu ya hatia ya mauaji ya kimbari ya dikteta wa zamani Efrain Rios Montt na kuamuru kesi yake iskilizwe upya.Hukumu hiyo imekuja siku kumi baada ya jopo la majaji watatu kumuona Rios Montt mwenye umri wa miaka 86 kuwa na hatia ya mauaji ya kimbari na uhalifu dhidi ya ubinaadamu kwa dhima aliyotimiza katika mauaji ya watu wa kabila la Mayan wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Guatemala. Majaji hao walisema kwamba alikuwa akijuwa juu ya mauaji ya zaidi ya watu 1,770 wa kabila asilia la Mayan katika milima ya magharibi mwa nchi hiyo lakini hakuchukuwa hatua yoyote ya kuzuwiya mauaji hayo. Jopo hilo la majaji lilimhukumu kifungo cha miaka 80 gerezani.
Kundi la viongozi wa wafanya biashara mashuhuri nchini Uingereza limeandika baruwa ya wazi kumtaka Waziri Mkuu mhafidhina David Cameron kuibakisha Uingereza katika Umoja wa Ulaya na kutokubali kusalimu amri kwa watu wenye mashaka na Umoja wa Ulaya waliomo ndani ya chama chake cha Conservative.Waliosaini baruwa hiyo akiwemo mkuu wa kampuni ya Virgin Sir richard Branson amesema kuwa mwanachama wa Umoja wa Ulaya kunaleta faida kubwa za kiuchumi kwa Uingereza zenye thamani ya zaidi ya euro bilioni 35 kwa mwaka. Baruwa hiyo inaunga mkono matakwa ya Cameron kuzungumzia masharti ya Uingereza kuendelea kuwa mwanchama wa umoja huo lakini imemtaka asiweke mbele masuala ya kisiasa dhidi ya yale ya kiuchumi. Malumbano juu ya suala hilo yamekigawa chama cha Conservative katika wiki za hivi karibuni.
Marekani imemteuwa mjumbe maalum kufuatilia na kupambana na chuki dhidi ya Uyahudi duniani kote.Hatua hiyo inakuja kufuatia repoti ya hivi karibuni kabisa ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani yenye kuelezea kwa kina kuwepo kwa matukio hayo nchini Venezuela, Misri na Iran.Waziri wa mambo ya nje wa Marekani John Kerry amemteuwa Ira Forman mkurugenzi wa muda mrefu wa Baraza la Taifa la Demokrasia la Wayahudi kuwa mjumbe maalum kupambana mwenendo huo wa chuki dhidi ya Uyahudi duniani kote.Forman anachukuwa nafasi ya Hannah Rosenthal ambaye alijiuzulu mwaka jana.Ripoti hiyo ya mwaka 2012 juu ya uhuru wa kuabudu imesema vyombo vya habari vya serikali nchini Venezuela vilichapisha taarifa mbali mbali za kupinga Uyahudi zilizomlenga mgombea wa urais Henrique Capriles Mkatoliki ambaye mababu zake walikimbia kutoka Poland kutokana na kuandamwa na chuki dhidi ya Uyahudi.
Kusikiliza matangazo ya Idhaa ya Kiswahili ya DW, tafadhali bonyeza alama ya spika ya masikioni hapo chini, na kuwasiliana nasi, tafadhali tuandikie moja kwa moja kupitia: kiswahili@dw.de.