1. Inhalt
  2. Navigation
  3. Weitere Inhalte
  4. Metanavigation
  5. Suche
  6. Choose from 30 Languages

Habari za Ulimwengu

Taarifa ya Habari za Ulimwengu kutoka Idhaa ya Kiswahili ya DW

News | 09.02.2012 | 03:57

Umoja wa Ulaya kuiwekea Syria vikwazo vikali

Umoja wa Ulaya - EU, utatangaza vikwazo vikali zaidi dhidi ya Syria, huku Urusi ikijaribu kuipatanisha serikali na upande wa upinzani ili kutuliza ghasia nchini humo. Urusi ambayo ni mshirika wa karibu wa Syria, na mataifa ya Magharibi, yanashinikiza njia tofauti katika kujaribu kukabiliana na hali ya umwagikaji wa damu nchini Syria ambayo imedumu kwa miezi 11 sasa. Afisa mkuu wa Umoja wa Ulaya alisema Umoja huo wenye nchi wanachama 27, hivi karibuni utaweka vikwazo vipya dhidi ya Syria huku ukilenga kuudhoofisha utawala wa Assad. Mjini New York Katibu Mkuu wa Umoja wa Mtaifa Ban Ki Moon aliwaambia waandishi wa habari kuwa Umoja wa Nchi za Kiarabu unapanga kuwarejesha waangalizi nchini Syria, na umeuomba Umoja wa Mataifa kuungana nao katika ujumbe huo. Ban alisema anasikitika  kwamba Baraza la Usalama lilishindwa kuzungumza kwa sauti moja kuhusiana na suala hilo la Syria, ili kusitisha umwagikaji wa damu. Amesema hatua hiyo imeipa nguvu serikali kuendelea na ukandamizaji wake dhidi ya raia wa Syria.

Urusi yasema umwagikaji wa damu usitishwe Syria

Na wakati ufumbuzi wa mzozo wa Syria ukiendelea kutafutwa, Urusi imesema kuwa juhudi za kutafuta njia ya kukomesha umwagikaji wa damu nchini Syria zinapaswa kuendelea ikiwa ni pamoja na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, lakini ikasisitiza kuwa uingiliaji wa mataifa ya nje haufai kuwa sehemu ya suluhisho hilo. Rais wa Urusi Dmitry Medvedev aliyasema hayo katika mashauriano ya simu na Waziri Mkuu wa Uturuko Tayyip Erdogan jana Jumatano. Miito ya kimataifa ya kumtaka Rais Bashar al Assad ajiuzulu imezidi kutolewa, lakini Urusi inaendelea kumuunga mkono. Wakati huo huo vikosi vya serikali kwa mara nyingine viliushambulia mji wa Homs, na kuauwa takriban raia 47 tangu Jumanne usiku.

Mazungumzo ya deni la Ugiriki yaendelea

Mazungumzo muhimu yanayolenga kuiepusha Ugiriki dhidi ya kufilisika yalifanywa mapema leo Alhamisi baada ya viongozi wa vyama vitatu vinavyoiunda serikali ya muungano kushindwa kukubaliana na masharti ya wakopeshaji ya kupunguzwa euro milioni 300 katika pensheni za serikali na za kibinafsi. Kulikuwa na maelewano mapana katika sehemu zote za mpango huo isipokuwa sehemu hiyo moja tu. Waziri mkuu wa Ugiriki Lucas Papademos amekutana leo Alhamis, na wawakilishi wa eneo la kanda ya sarafu ya euro, na Shirika la Fedha Ulimwenguni - IMF. Mkutano wa jana uliodumu saa nane, ulikamilika bila ya muafaka kuhusu hatua mpya za kubana matumizi. Mpango huo ni pamoja na kupunguzwa kwa asilimia 20 kima cha chini cha mishahara, na unazifuta karibu nafasi 15,000 za ajira katika sekta ya umma. Hatua hizo zinahitajika ili Ugiriki iweze kupokea kitita cha uokozi cha euro bilioni 130. Mawaziri wa fedha wa nchi zinazotumia sarafu ya euro wanatarajiwa kukutana hii leo mjini Brussels ili kuijadili hali hiyo ya Ugiriki.

Al Shabaab wakiri kushambulia Mogadishu

Nchini Somalia, wanamgambo wa Al Shabaab wamekiri kuhusika na shambulizi la kujitoa muhanga katika hoteli ya Muna, kwenye eneo lililo na ofisi nyingi za serikali katika mji mkuu Mogadishu. Mripuko huo uliwauwa watu tisa, na ukawajeruhi wengine kadhaa, wakiwemo mwezi wa Agosti mwaka wa 2010, na kuwauwa watu 32 wakiwemo wabunge sita. Wakati huo huo Umoja wa Ulaya - EU, umetishia kusitisha huduma za msaada nchini Somalia, hadi pale viongozi wa nchi hiyo watakaposhinikiza kufanywa mageuzi ya kisiasa. Mjumbe wa EU katika upembe wa Afrika Alexander Rondos ameliambia shirika la habari la Reuters kwua Umoja huo unasikitishwa na mwendo wa kujikokota wa mageuzi katika mfumo wa kisiasa nchini Somalia, licha ya unafisi mkubwa wa kijeshi kupatikana katika vita dhidi ya wanamgambo wenye mafungamano la al Qaeda. EU ni mfadhili mkubwa wa msaada nchini Somalia.

Asimilia 90 ya Mto Danube yaganda barafu

Wimbi la baridi kali linazidi kuyakumba maeneo kadhaa ya bara la Ulaya. Nchi nne za eneo la Balkan zimesitisha shughuli zake za uchukuzi wa meli katika mto Danube, huku asilimia 90 ya njia hiyo ya majini yenye kilomita 3,000 ikifungwa na barafu inayoelea juu ya maji. Serbia imesema jeshi lake linatumia mabomu ya kuvunja barafu katika mto huo wa Danube. Usafiri wa meli pia umesitishwa nchini Bulgaria, Croatia na Romania. Mamia ya watu wamekufa katika sehemu kadhaa barani Ulaya huku viwango vya joto vikishuka kabisa hadi nyuzi 45 sentigredi chini ya sifuri.

Safari za ndege Ufaransa zavurugwa kufuatia mgomo wa marubani

Usafiri wa angani nchini Ufaransa ulitatizika kwa kiwango kikubwa tena jana Jumatano, huku marubani wakiendelea na mgomo wao wa siku tatu. Shirika la safari za ndege la Ufaransa - Air France lilisema lilifutilia mbali asilimia 40 ya safari zake za masafa marefu, na asilimia 30 ya safari za maeneo ya karibu. Mgomo huo ni wa kulalamikia mswada ambao utahitaji kutolewa makataa ya saa 48 kabla ya mgomo wowote wa wafanyakazi wa sekta ya safari za ndege. Shirika hilo linapendekeza kuwa abiria wahairishe safari zao zilizopangwa leo hadi kesho Ijumaa, wakati mgomo huo unatarajiwa kuisha.

Zambia na Cote d'ivoire kukutana katika fainali ya kombe la mataifa ya bara la Afrika

Michezoni Zambia na Cote d'ivoire zitakutana katika fainali ya kombe la mataifa ya bara la Afrika baada ya kushinda mechi zao za nusu fainali hapo jana. Zambia waliizuia fainali ambayo wengi walitaraji kuiona kati ya Ghana na Cote d'ivoire wakati walipowaduwaza The Black Stars goli moja kwa nunge, kufuatia bao lake Emmanuel Mayuka, huku nao Cote d'ivoire wakiwachapa Mali kwa goli hilo moja kupitia bao lake Gervinho katika kipindi cha kwanza. Hivyo Ghana na Mali zitakabana koo siku ya Jumamosi mjini Malabo, ili kumtafuta mshindi wa nafasi ya tatu kabla ya fainali kusakatwa Jumapili mjini Libreville.

Capello ajiuzulu kama kocha wa Uingereza

Fabio Capello amejiuzulu kama mkufunzi wa timu ya taifa ya soka ya Uingereza. Katika tangazo lililotolewa jana jioni, chama cha soka nchini Uingereza FA kilisema raia huyo wa Italia alijiuzulu kufuatia mzozo kuhusiana na chama hicho cha soka, ambacho wiki iliyopita kilimpokonya John Terry unahodha wa timu ya taifa ya Uingereza. Capello amekuwa kocha wa Uingereza tangu mwaka wa 2007.

Unaweza kusikiliza matangazo yetu hapa

Kusikiliza matangazo ya Idhaa ya Kiswahili ya DW, tafadhali bonyeza alama ya spika ya masikioni hapo chini, na kuwasiliana nasi, tafadhali tuandikie moja kwa moja kupitia: kiswahili@dw.de.

Maoni kutoka DW wiki hii yanajadili hatima ya kisiasa ya Kenya baada ya uamuzi wa ICC