1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wabunge waidhinisha urafushaji wa msaada kwa Ugiriki

Admin.WagnerD27 Februari 2015

Wabunge wa Ujerumani wanatazamiwa kuidhinisha urefushaji wa mpango wa uokozi wa Ugiriki katika kura ya bungeni siku ya Ijumaa,na hivyo kuondoa kizingiti cha mwisho cha kuendeleza musaada muhimu ukitiririka mjini Athens.

https://p.dw.com/p/1Eicc
Deutschland Wolfgang Schäuble Debatte zur Griechenland Hilfe
Picha: Reuters/H. Hanschke

Msimamo usiyoyumba wa serikali mjini Berlin, juu ya haja ya Ugiriki kutekeleza mageuzi ya kiuchumi ili ipatiwe msaada zaidi unaungwa mkono katika miji mikuu mingine, kuanzia Helsinki nchini Finland, hadi wapokeaji wa zamani wa msaada wa uokozi, Madirid nchini Uhispania na Lisbon nchini Ureno.

Lakini matamshi makali kutoka mlipaji mkuu wa Ulaya Ujerumani yamesababisha majibizano makali na serikali mjini Athens tangu uchaguzi wa mwezi uliopita ulipoiingiza madarakani serikali ya siasa za mrengo mkali wa kushoto ya Waziri Mkuu Alexis Tsipras, kufuatia hasira za wananchi waliochoshwa na miaka kadhaa ya kubana matumizi.

Waziri wa fedha wa Ujerumani Wolfgang Schaeble akiwa bungeni kutetea hatua ya kurefusha mpango wa uokozi kwa Ugiriki.
Waziri wa fedha wa Ujerumani Wolfgang Schaeble akiwa bungeni kutetea hatua ya kurefusha mpango wa uokozi kwa Ugiriki.Picha: Reuters/H. Hanschke

Hata wakati waziri wa fedha wa Ujerumani anaelemea zaidi Ulaya Wolfgang Schaeuble akiwasihi wabunge wa muungano wake wa wahafidhina kuunga mkono urefushaji wa mpango huo wa uokozi siku ya Alhamisi, mwenyewe alieleza kushangazwa na matamshi mapya ya mwezake wa Ugiriki kuhusu deni la nchi hiyo.

Mzigo mzito kwa Ugiriki

Shinikizo kutoka deni la Ugiriki la euro bilioni 320 -- ambalo ni sawa na asilimia 175 ya uzalishaji wake wa kila mwaka wa kiuchumi -- ni kubwa mno, kiasi kwamba waziri mkuu Tsipras anataka kujadili upya ulipaji wa deni hilo wakati wa miezi minne ya urefushaji wa mpango wa sasa.

Ujerumani ndiyo mshirika pekee wa Ugiriki katika kanda inayotumia sarafu ya euro, kufanya kura ya bungeni juu ya kuipatia Ugiriki nafasi ya kupumua, inayolenga kuepuka janga la muda wa mwisho siku ya Jumamosi, ambao unaweza kusababisha nchi hiyo kuondoka katika kanda inayotumia sarafu ya euro.

Licha ya wasiwasi miongoni mwa baadhi ya wabunge, hatua hiyo inatarajiwa kupita katika Bundestag, ambako mjadala unaendelea muda huu, na ambako muungano wa Kansela Angela Merkel una wingi usiyo na mashaka.

Wabunge wengi wanakubali, japokuwa wana walakini, alisema Gunther Krichbaum, mhafidhina na mwenyekiti wa kamati ya masuala ya Ulaya katika Bundestag, na kuongeza kuwa wabunge hawako tayari kutoa tahfifu zaidi.

Waziri wa fedha wa Ugiriki Yanis Varoufakis, profesa wa uchumi anaesifika kwa kuwa muwazi, alipandisha tena joto nchini Ujerumani siku ya Jumatano kwa kutaka uwepo mjadala, kuanza mara moja kujadili upya mzigo wa madeni ya taifa lake.

"Tupeni nafasi ya kurejesha utulivu na tuanze kukuza uchumi, na hapo tutaanza kufanya mageuzi kwa sababu tunataka kufanya mageuzi, siyo kwa sababu mnatutaka kufanye mageuzi,"alisema waziri wa fedha wa Ugiriki Yanis Voraufakis, profesa wa uchumi anaesifika kwa kuwa muwazi.

Kansela Angela Merkel na naibu wake Sigmar Gabriel wakifuatilia kwa makini mjadala bungeni.
Kansela Angela Merkel na naibu wake Sigmar Gabriel wakifuatilia kwa makini mjadala bungeni.Picha: Reuters/H. Hanschke

Raia wachache wanaunga mkono

Uchunguzi wa maoni uliyochapishwa wiki hii unaonyesha kuwa asilimia 21 tu ya Wajerumani ndiyo wanaunga mkono bunge la hiyo kuidhinisha ahueni kwa Ugiriki. Shirika la fedha la kimataifa IMF na benki kuu ya Ulaya ECB, ambazo kwa pamoja na mataifa wanachama wa kanda ya euro wanachangia sehemu kubwa ya msaada kwa Ugiriki, yameelezea mashaka

Alexander Kritikos, mkurugenzi w autafiti katika taasisi ya kiuchumi ya DIW ya Ujerumani, alisema Wagiriki wana tabia ya zamani ya kuelekeza hasira zao kwa waziri Schaeuble peke yake, lakini mataifa mengine kama vile Finland, Uholanzi na mataifa ya Baltic yalichukuwa msimamo sawa.

Mwandishi: Iddi Ssessanga/afpe, dpae
Mhariri: Mohammed Khelef