1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bayern Munich yaanza vibaya sehemu ya pili ya msimu

31 Januari 2015

Mabingwa wa Ujerumani Bayern Munich wameanza vibaya sehemu ya pili ya msimu baada ya mapumziko ya kipindi cha baridi, kwa kubugizwa magoli 4-1 na Wolfsburg iliyo katika nafasi ya 2, kwenye mechi pekee ya jana usiku.

https://p.dw.com/p/1ETjD
Wachezaji wa Bayern Munich wakitafakari kipigo walichokipata
Wachezaji wa Bayern Munich wakitafakari kipigo walichokipataPicha: Getty Images/M. Rose

Haikuwa siku njema kwa mabingwa hao wanaofundishwa na Kocha Pep Guardiola, ambao hadi wanakwenda mapumziko walikuwa hawajashindwa mechi yoyote msimu huu. Kwa muda wa dakika tisini tu, Wolfsburg ilikuwa imewabugiza magoli 4, idadi sawa na magoli iliyofungwa Bayern Munich katika mechi 17 za sehemu ya kwanza ya msimu huu.

Mnamo dakika ya tatu tu ya mchezo mholanzi Bas Dost aliunganisha pasi iliyochongwa na Daniel Caliguiri, na kuachia mkwaju ambao kipa Manuel Neuer wa Bayern Munich aliusindikiza kwa macho hadi kwenye kona ya wavu. Juhudi za Bayern kutaka kuzawazisha ziliishia pachungu, baada ya Wolfsburg kuwageuzia kibao, katika shambulizi lililohitimishwa kwa goli la pili lililotiwa kimiani na yule yule Bas Dost.

Mkuki kwa nguruwe, kwa binadamu mchungu

Magoli mawili kwa nunge yaliwafanya wachezaji wa Bayern ambao hawakuzoea kujikuta katika hali hiyo wakipoteza subira, na kucheza rafu iliyopelekea kadi ya njano kwa kiungo wao Xabi Alonso, ambaye alionekana kupandwa na jazba. Hadi mapumziko ubao wa magoli ulionyesha Wolfsburg 2, Bayern Munich 0.

Kwa VFL Wolfsburg ilikuwa ni sherehe
Kwa VFL Wolfsburg ilikuwa ni sherehePicha: Getty Images/M. Rose

Kama mabingwa hao walidhani watarekebisha mambo katika kipindi cha pili ilikuwa ni ndoto tu, kwani ilikuwa Wolfsburg iliyoliona lango tena mnamo dakika ya 53 ya mchezo, kupitia mbelgiji Kevin de Bruyne, aliyekimbia nusu ya uwanja, na kumtumia salamu kipa Neuer kwa nduki kutoka umbali wa mita kumi.

Magoli matatu kwa sufuri ugenini yaliufanya mlima wa Bayern Munich kuwa mrefu, lakini kwenye dakika ya 55 Juan Bernat aliweza kurudisha bao moja ambalo liliishia kuwa pekee la kufutia machozi. Haikuishia hapo kwani kauli ya mwisho ilitoka kwa Wolfsburg mnamo dakika ya 73, pale yule yule Kevin de Bruyne aliposhindilia msumari wa mwisho kwenye jeneza la Bayern Munich kwenye mechi hiyo kwa kupachika bao la nne.

Guardiola akubali kipigo

Akizungumza na waandishi wa habari baaya ya mechi, kocha wa Bayern Munich Pep Guardiola hakuwa na ukaidi. ''Ni kweli walikuwa timu bora na walistahili ushindi'' alisema Guardiola, na kuongeza kuwa magoli yao yaliingia katika muda mbaya kwa Bayern, yaani dakika za mwanzoni na za mwishoni.

Kocha wa Bayern Munich Pep Guardiola
Kocha wa Bayern Munich Pep GuardiolaPicha: Getty Images

Kwa upande mwingine, kocha wa Wolfsburg Dieter Hecking amewapongeza vijana wake, akisema ushindi huu unawapa ari ya kuendelea kufanya vyema.

Kongo dhidi ya Kongo katika kombe la Afrika la Mataifa

Na katika michuano ya kombe la Afrika la Mataifa ambayo hii leo inaingia katika raundi ya robo fainali zitachezwa mechi mbili jioni ya leo, ya kwanza ikiwa kati ya watani wa jadi, Kongo Kinshasa na Kongo Brazzaville, ya pili itakuwa kati ya Tunisia, na wenyeji Guinea ya Ikweta.

Akizungumzia mechi dhidi ya watani wao wa Congo Brazzaville, kocha wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Florent Ibenge, amesema ni mchezo kati ya ndugu wanaotenganishwa tu na mto Kongo. Kocha wa Kongo Brazzaville Claude Le Roy ambaye siku za nyuma aliifunza Kongo Kinshasa ameunga mkono kauli ya mpinzani wake, akisema utakuwa mchuano baina ya ndugu wanaojuana vyema, na kwamba hilo litaongeza msisimko.

Mwandishi: Daniel Gakuba/afpe/ape

Mhariri: Sudi Mnette